NOVENA KWA MWENYE HERI YOSEFU ALLAMANO

KISWAILI

 

Novena:

Siku ya kwanza

 

TWATEGEMEA SANA

WEMA WA MUNGU

 

"Ombeni, nanyi mtapewa; tafuteni,

nanyi mtaona; bisheni, nanyi mtafunguliwa;

kwa maana kila aombaye

hupokea, naye atafutaye huona, naye

abishaye atafunguliwa" (Mt 7:7-8).

 

Baba mwema, Mwenye Heri Yosefu

Allamano alionja maishani mwake upendo

wako wenye huruma na anatuhimiza

kusali kwa imani kubwa, bila kuwa na "hofu ya

kutopata tunaloomba", kwani wewe "yote

huwajalia wanaokuamini". Kwa tumaini

kubwa na moyo wa ki-mwana, tunaukimbilia

wema wako wa kibaba na, kwa

maombezi ya Mtumishi wako mwaminifu,

tunakuomba neema ya...

Kama wana Kanisa, tunakuomba upeleke watenda

kazi wengi katika shamba lako, ili

kueneza Neno la wokovu hadi miisho ya

dunia (rej. Mdo 1:8). Kwa Kristo Bwana

wetu. Amina.

 

Baba yetu,…

Salamu Maria,…

Atukuzwe,…

Bikira Maria Consolata, utuombee.

 

 

 

Siku ya pili

 

TUMWAMINI MUNGU

APENDAYE KUTUSAIDIA

 

"Nanyi mkiwa katika kusali, msipayukepayuke,

kama watu wa mataifa;

maana wao hudhani ya kuwa

watasikiwa kwa sababu ya maneno

yao kuwa mengi. Maana Baba yenu

anajua mnayohitaji kabla ninyi hamjamwomba" (Mt 6:7-8).

 

Baba yetu, Mwenyeheri Yosefu Allamano

alielewa vizuri juhudi zako kwa wanao

wote, hasa wenye shida, na anatuhakikishia

"kuwa yeyote akuaminiye hatafadhaika kamwe" kwani

"wewe huweza, hujua na hupenda kutusaidia."

Maneno haya yanatutia moyo na

kutuwezesha kukuomba kwa imani kubwa

katika wema wako usio na mwisho.

Kwa maombezi ya Mtumishi wako mwaminifu,

tunakuomba neema ya...

Pamoja na wote wakuaminio, tunakuomba

sana ueneze Ufalme wako wa upendo

na amani ulimwenguni kote (rej. Mt

24:14). Kwa Kristo Bwana wetu. Amina.

 

Baba yetu,…

Salamu Maria,…

Atukuzwe….

Bikira Maria Consolata, utuombee.

 

 

 

 

Siku ya tatu


MATUMAINI KATIKA

MAJALIWA YA BABA

 

" Waangalieni ndege wa angani, ya

kwamba hawapandi, wala hawavuni,

wala hawakusanyi ghalani; na Baba

yenu wa mbinguni huwalisha hao.

Ninyí je, si bora kupita hao?" (Mt

6:26).

 

Baba Mjaliwa, Mwenye Heri Yosefu

Allamano alipata kuona msaada wako siku

zote za maisha yake na anathibitisha

kuwa “tusisite kutumainia majaliwa

yako", kwani "wewe, unayewalisha ndege,

hakika utatujalia na sisi kwa wingi."

Tunakukimbilia wewe uliye karibu nasi

daima na uliye mwangalifu kwa mahitaji

yetu. Kwa maombezi ya Mtumishi wako

mwaminifu, tunakuomba kwa imani ya

ki-mwana neema ya...

Tukiungana na wabatizwa wote, tunaomba

ili Kanisa lako lienee na kukua kati ya

mataifa yote na, kama chachu ilivyo katika

unga, liyabadilishe kwa nguvu ya Injili

(rej. Lk 13:20-21). Kwa Kristo Bwana

wetu. Amina.

 

Baba yetu,…

Salamu Maria,…

Atukuzwe….

Bikira Maria Consolata, utuombee.

 

 

 

 

Siku ya nne


TUMWAMINI

MUNGU BILA HOFU

 

"Mkimwomba Baba neno lolote

atawapa kwa jina langu. Ombeni,

nanyi mtapata, furaha yenu iwe timilifu"

(Yn 16.23-24).

 

Baba mwaminifu sana kwa kila ahadi,

Mwenyeheri Yosefu Allamano alikuamini daima,

wewe uliye mwangalifu kwa viumbe

vyako, na unatushauri "kuweka yote

mikononi mwako, bila hofu, kwani wewe

huachi kazi zako bila kuzikamilisha," wala

hughairi matumaini wanayokutumainia

wana wako. Tukiwa na hakika hii ya

kwamba daima unasikiliza maombi yetu,

tunajitolea kwako kabisa na, kwa

maombezi ya Mtumishi wako mwaminifu, tunakuomba

neema ya...

Tukiungana na Kanisa la kimisionari ulimwenguni kote,

tunakuomba ili Mwana wako, uliyemtuma

kuuokoa ulimwengu wote (rej. Yn 3:17),

ajulikane na watu wote kama Mchungaji

Mwema na hatimaye duniani pawepo

na kundi moja na mchungaji mmoja

(rej. Yn 10:16). Kwa Kristo Bwana wetu.

Amina.

 

Baba yetu,… Salamu Maria,… Atukuzwe,...

Bikira Maria Consolata, utuombee.

 

 

 

 

Siku ya tano


NILIMTUMAINIA MUNGU

 

"Je, mashomoro watano hawauzwi

kwa senti mbili? Wala hasahauliwi

hata mmojawapo mbele za Mungu.

Lakini hata nywele za vichwa vyenu

zimehesabiwa zote. Msiogope basi,

bora ninyi kuliko mashomoro wengi"

(Lk 12:6-7).

 

Baba Mwenyezi wa huruma, Mwenye

Heri Yosefu Allamano hakukosa kutumainia

msaada wako katika kila hitaji, na

anatufundisha "kuendelea kuuamini upendo

wako bila kukata tamaa, hata tusipopata

yote", ama "inapotubidi kusubiri, ili

kutujaribu na kutukumbusha kuwa sisi ni

maskini."

Kwa dhana hii moyoni, tunadhihirisha

imani yetu ya siku zote katika

moyo wako wa Baba na, kwa maombezi

ya Mtumishi wako mwaminifu, tunakuomba

neema ya...

Kwa ajili ya wale wasiokufahamu bado,

tunakuomba uwasindikize watangazaji wa

Injili, ili jina lako takatifu lijulikane na

kusifiwa duniani kote (rej. Mdo 2:21).

Kwa Kristo Bwana wetu. Amina.

 

Baba yetu,…

Salamu Maria,…

Atukuzwe,…

Bikira Maria Consolata, utuombee.

 

 

 

 

Siku ya sita


TWASADIKI WEMA WA

BWANA

 

"Basi ikiwa ninyi, mlio waovu, mnajua

kuwapa watoto wenu vipawa vyema,

je, si zaidi sana Baba yenu aliye mbinguni

atawapa mema wao wamwombao?"

(Mt 7:11).

 

Baba mwema, Mwenyeheri Yosefu

Allamano alithibitisha kuwa ukarimu

wako hauna kifani, na anatuhakikishia

kuwa "wewe ungependa sisi tuwe na

imani katika wema wako", tuweze "kuja

kwako hata katika jambo dogo na kukutumainia

wewe peke yako, bila kujali

matukio yajayo". Tukiamini ukarimu

wako, tunakujia wewe uliye mwema sana

na, kwa maombezi ya Mtumishi wako

mwaminifu, tunakuomba neema ya...

Kwa kufuata mfano wa Mwana wako

ambaye, ingawa alikuwa Mungu,

alijifanya kuwa hana utukufu,

akatwaa hali ya mtumwa, akawa mtii

hata mauti ya msalaba (rej. Flp 2:7-8),

Kanisa lijue kujishughulikia zaidi na zaidi

kwa ajili ya wanaoteseka kwa sababu ya

umaskini, vita na ukosefu wa kila aina wa

haki. Kwa Kristo Bwana wetu. Amina.

 

Baba yetu,… Salamu Maria,… Atukuzwe,...

Bikira Maria Consolata, utuombee.

 

 

 

 

Siku ya saba


UJASIRI WA KUSALI

WATOKANA NA IMANI

 

"Mkiwa na imani, msipokuwa na

shaka, hata mkiuambia mlima huu:

Ng'oka, ukatupwe baharini, litatendeka.

Na yoyote mtakayoyaomba katika

sala mkiamini, mtapokea." (Mt 21:21-

22).

 

Baba, upokeaye maombi ya wanao,

Mwenyeheri Yosefu Allamano, ili apate

msaada kwako, alionesha daima ustahimilivu

mkubwa na anatufundisha kuwa "ili

tupate neema tunapaswa kuiomba kwa

imani kubwa, kwa ujasiri ule wa kuweza

kutenda miujiza," na kututia moyo kwa

maneno haya: "Jipeni moyo kila

wakati na tusonge mbele katika Bwana."

Tukijipa moyo kwa mafundisho yake,

tunakujia wewe unayetutunza kwa upendo

na, kwa maombezi ya Mtumishi wako

mwaminifu, tunakuomba neema ya...

Tukiungana na watu wote wenye mapenzi

mema, tunakusihi toka mawio ya jua hata

machweo yake uwakusanye watoto wako

wote waliotawanyika na uwakaribishe katika

karamu ya Ufalme wako (rej. Mt 8:11).

Kwa Kristo Bwana wetu. Amina.

 

Baba yetu,… Salamu Maria,… Atukuzwe,...

Bikira Maria Consolata, utuombee.

 

 

 

 

Siku ya nane


TUENDELEE KUTARAJIA

YASIYOWEZA KUTARAJIWA

 

"Msisumbuke, basi, mkisema: Tule

nini? au Tunywe nini? au Tuvae nini?

Kwa sababu Baba yenu wa mbinguni

anajua ya kuwa mnahitaji hayo yote.

Basi msisumbuke ya kesho" (Mt 6:31-

34).

 

Baba, unayetoa tunu za kustaajabisha,

Mwenyeheri Yosefu Allamano, Nata katika

nyakati zilizo ngumu katika maisha, alitarajia

yasiyoweza kutarajiwa (rej. Rum

4:18) na anatuonya "tuwe na tumaini lililo

hai moyoni, tuwe na tumaini kubwa

kabisa, kwani anayetumaini kidogo tu

anakukosea wewe", uliye na wema bila

mipaka. Tukifuata mfano wake mzuri,

tunapenda kukuonesha tumaini letu

kubwa katika ukarimu wako wa kibaba na,

kwa maombezi ya Mtumishi wako

mwaminifu, tunakuomba neema ya...

Tukiamini ya kuwa unataka "watu wote

waokolewe, na kupata kujua yaliyo kweli"

(1Tim 2:4), tunakusihi sana utume mwanga

wa Roho wako, ili "kila ulimi ukiri ya

kuwa Yesu Kristo ni Bwana" (Fip 2: I 1).

Kwa Kristo Bwana wetu. Amina.

 

Baba yetu,… Salamu Maria,… Atukuzwe,...

Bikira Maria Consolata, utuombee.

 

 

 

 

Siku ya tisa


MAPENZI MATAKATIFU

YA MUNGU YAFANYIKE

 

"Basi ninyi hivi sasa mna huzuni; lakini

mimi nitawaona tena, na mioyo

yenu itafurahi, na furaha yenu hakuna

awaondoleaye. Tena siku ile hamtaniuliza

neno lolote" (Yn 16:22-23).

 

Baba, Mungu wetu, Mwenyeheri Yosefu

Allamano, akifuata mfano wa Mwana

wako mpendwa, alitenda daima yaliyokupendeza

(rej. Yn 8:29) na anatufundisha ya

kuwa "upo katika yote, hata yaliyo madogo

na kuyatawala kwa manufaa yetu, ukituomba

kutii kwa moyo amri zako za upendo".

 

Tukithibitisha utayari wetu wa kutimiza

kwa moyo mapenzi yako matakatifu, yoyote

yale yatakayokuwa, hatusiti kuendelea

kukuomba, kwa tumaini lile lile, kutujalia

kwa upendo neema ya...

Kwa nguvu ya imani yetu ya kikristo,

tunakuomba sana ili familia nzima ya mwanadamu

iweze kumtambua Kristo kama

Mwokozi wa pekee wa ulimwengu, yeye

anayeishi na kutawala nawe, katika umoja

wa Roho Mtakatifu, daima na milele (rej.

Yn 4:42). Amina.

 

Baba yetu,… Salamu Maria,… Atukuzwe,...

Bikira Maria Consolata, utuombee.

 

 

 

 

Sala ya mwisho


SHUKRANI

 

Ee Baba, chemchemi ya kila kilicho

chema, wimbo wetu wa sifa upae kwako

kwa ajili ya mapaji uliyomjalia Mwenye

Heri Yosefu Allamano.

Katika Kanisa lako alikuwa kuhani wa

agano jipya, mhudumu wa faraja, mshauri

mwenye busara na hekima, mwenye

kutafuta daima mapenzi yako.

Baba Allamano, mwenye bidii kwa ujio

wa ufalme wako, akawa Baba na Kiongozi

wa Familia za Watawa Wamisionari

pamoja na Maria, mmisionari wa kwanza

wa Injili, wamtangaze duniani kote Kristo

Mkombozi.

Ee Mungu Baba, utujalie kuiga mfano

wake na kushiriki katika kazi ya

Ukombozi, ili watu wote wawe na uzima,

kisha wawe nao tele.

Kwa Kristo Bwana wetu. Amina

giuseppeallamano.consolata.org